Saturday, March 3, 2012

MGAMBO WA JIJI


Kuna jamaa mmoja alikuwa anajisaidia haja ndogo sehemu ambayo hairuhusiwi, wakati akikamilisha zoezi lake hilo, mgambo wa jiji alitokea na kutaka kumkamata.

“Samahani ndugu unajisaidia sehemu isiyoruhusiwa, kwa nini?”
“Nioneshe choo.”
“Unajitia jeuri siyo, maliza kujisaidia uzungumze na jamhuri.”
“Poa.”

Jamaa baada ya kuelezwa vile aliacha alipokuwa akikojoa mwanzo na kusogea mbele kukojoa sehemu nyingine, jambo lililowafanya mgambo wa jiji kuhoji:

“Wewe vipi mbona unazidi kuchafua mazingira, huoni kama unaongeza kosa?”
“Si ndiyo nizungumze vizuri na jamhuri?”

Mgambo wa jiji alizidi kukasirika na kumsubiri jamaa kwa hamu, jamaa alipomaliza kujisaidia alimgeukia mgambo aliyekuwa na rungu mkononi.

“Haya, mlete jamhuri nizungumze naye nimuulize vyoo vipo wapi?”
Jamaa alipotaka kumkamata, aligoma, ilibidi kiongozi wao asogee na kutaka kujua kulikoni. Mgambo alimwambia kiongozi wake kamkuta jamaa anachafua mazingira. Jamaa alijitetea:

“Mkuu nimemkuta kijana wako akijisaidia hapa na mimi nikajisaidia pembeni yake, sasa nashangaa ananikamata.”
“Muongo?” Mgambo alijitetea.

“Kama nadanganya huo mkojo mwingine wa nani?”
Mkuu wa mgambo alipoangalia kweli aliona kuna sehemu mbili ambazo zote zilikuwa bado mkojo mbichi.

Aliamini kabisa yule jamaa anasema kweli na kuamua kumuachia. Jamaa aliondoka huku akichelekea moyoni kwa kumzidi akili mgambo wa jiji. Kweli akili ni nywele.



Courtesy : The GlobalPublishers